Yer. 51:42-62 Swahili Union Version (SUV)

42. Bahari imefika juu ya Babeli,Umefunikwa kwa wingi wa mawimbi yake.

43. Miji yake imekuwa maganjo;Nchi ya ukame, na jangwa;Nchi asimokaa mtu ye yote,Wala hapiti mwanadamu huko.

44. Nami nitafanya hukumu juu ya Beli katika Babeli, nami nitavitoa katika kinywa chake alivyovimeza; wala mataifa hawatamwendea tena; naam, ukuta wa Babeli utaanguka.

45. Enyi watu wangu; tokeni katikati yake, mkajiokoe nafsi zenu na hasira kali ya BWANA, kila mmoja wenu.

46. Wala isizimie mioyo yenu, wala msiiogope habari itakayosikiwa katika nchi; maana habari itakuja mwaka mmoja, na baadaye mwaka wa pili habari itakuja, na udhalimu katika nchi, mwenye kutawala akishindana na mwenye kutawala.

47. Basi angalia, siku zitakuja, ambazo katika siku hizo, nitafanya hukumu juu ya sanamu za Babeli, na nchi yake yote itatahayarika; na watu wake wote waliouawa wataanguka katikati yake.

48. Ndipo mbingu, na nchi, na vitu vyote vilivyomo, vitaimba kwa furaha juu ya Babeli; kwa maana watu waangamizao watamjilia kutoka kaskazini, asema BWANA.

49. Kama vile Babeli alivyowaangusha watu wa Israeli waliouawa, ndivyo watakavyoanguka katika Babeli watu wa nchi yake nzima waliouawa.

50. Ninyi mliojiepusha na upanga,Enendeni zenu, msisimame;Mkumbukeni BWANA tokea mbali,Na Yerusalemu ukatiwe mioyoni mwenu.

51. Twaona haya kwa kuwa tumesikia mashutumu;Fedheha imetufunikiza nyuso zetu;Kwa sababu wageni wamepaingiaPatakatifu pa nyumba ya BWANA.

52. Kwa sababu hiyo siku zinakuja, asema BWANA, nitakapozihukumu sanamu zake; na katika nchi yake yote waliojeruhiwa wataugua.

53. Babeli ujapopanda mbinguni, na ujapopafanya mahali pa juu penye nguvu zake kuwa ngome, hata hivyo toka kwangu wenye kuangamiza watamwendea, asema BWANA.

54. Sauti ya kilio kutoka Babeli,Na ya uangamivu mkuu toka nchi ya Wakaldayo!

55. Maana BWANA amwangamiza Babeli,Na kuikomesha sauti kuu ndani yake;Na mawimbi yake yavuma kama maji mengi,Mshindo wa sauti zao wafanya makelele;

56. Kwa maana mwenye kuangamiza amefika kwake;Naam, amefika Babeli;Na mashujaa wake wametwaliwa;Pinde zao zimevunjika kabisa;Maana BWANA ni Mungu wa kisasi;Hakika yake yeye atalipa.

57. Nami nitawalevya wakuu wake, na watu wake wenye hekima, maliwali wake, na maakida wake, na mashujaa wake; nao watalala usingizi wa milele, wasiamke, asema Mfalme, BWANA wa majeshi, ambaye jina lake ni BWANA.

58. BWANA wa majeshi asema hivi, Kuta pana za Babeli zitabomolewa kabisa, na malango yake marefu yatateketezwa; nao watu watajitaabisha kwa ubatili, na mataifa kwa moto; nao watachoka.

59. Neno ambalo Yeremia, nabii, alimwamuru Seraya, mwana wa Neria, mwana wa Maaseya, alipokwenda Babeli pamoja na Sedekia, mfalme wa Yuda, katika mwaka wa nne wa kumiliki kwake. Basi Seraya alikuwa msimamizi mkuu wa nyumba ya mfalme.

60. Naye Yeremia akaandika katika kitabu habari ya mabaya yote yatakayoupata Babeli, maneno hayo yote yaliyoandikwa juu ya Babeli.

61. Naye Yeremia akamwambia Seraya, Utakapofika Babeli, basi angalia uyasome maneno haya yote,

62. ukaseme, Ee BWANA, umenena habari za mji huu kwamba utakatiliwa mbali, usikaliwe na awaye yote, wala wanadamu wala wanyama, lakini uwe ukiwa hata milele.

Yer. 51