2 Nya. 29:19-32 Swahili Union Version (SUV)

19. Tena vyombo vyote alivyovitupa mfalme Ahazi alipotawala, hapo alipoasi, tumevitengeza na kuvitakasa; navyo, tazama, vipo mbele ya madhabahu ya BWANA.

20. Ndipo Hezekia mfalme akaamka mapema, akakusanya wakuu wa mji, akapanda nyumbani kwa BWANA.

21. Wakaleta ng’ombe waume saba, na kondoo waume saba, na wana-kondoo saba, na mabeberu saba, kuwa sadaka ya dhambi kwa ajili ya ufalme, na kwa ajili ya patakatifu, na kwa ajili ya Yuda. Akaamuru makuhani, wana wa Haruni, wawatoe madhabahuni pa BWANA.

22. Basi wakawachinja ng’ombe, na makuhani wakaipokea damu, wakainyunyiza madhabahuni; wakawachinja kondoo waume, na kuinyunyiza damu madhabahuni; wakawachinja na wana-kondoo, na kuinyunyiza damu madhabahuni.

23. Wakawaleta karibu mabeberu wa sadaka ya dhambi mbele ya mfalme na kusanyiko; wakawawekea mikono yao;

24. na makuhani wakawachinja, wakaitoa damu yao kuwa sadaka ya dhambi madhabahuni, ili kuwafanyia Israeli wote upatanisho; maana mfalme aliamuru Israeli wote wafanyiwe sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya dhambi.

25. Akawasimamisha Walawi nyumbani mwa BWANA wenye matoazi, wenye vinanda, na wenye vinubi, kama alivyoamuru Daudi, na Gadi mwonaji wa mfalme, na Nathani nabii; kwani BWANA aliamuru hivi kwa manabii wake.

26. Wakasimama Walawi wenye vinanda vya Daudi, na makuhani wenye mapanda.

27. Hezekia akaamuru kutoa sadaka ya kuteketezwa madhabahuni. Na wakati ilipoanza sadaka hiyo ya kuteketezwa, ukaanza na huo wimbo wa BWANA, na mapanda, pamoja na vinanda vya Daudi mfalme wa Israeli.

28. Na kusanyiko lote wakaabudu, waimbaji wakaimba, wenye mapanda wakapiga; haya yote yakaendelea hata ilipomalizika sadaka ya kuteketezwa.

29. Hata walipokwisha kutoa sadaka, mfalme, na hao wote waliokuwapo naye, wakasujudia, wakaabudu.

30. Tena Hezekia mfalme na wakuu wakawaamuru Walawi, wamwimbie BWANA sifa kwa maneno ya Daudi, na ya Asafu mwonaji. Wakaimba sifa kwa furaha, wakainama vichwa, wakaabudu.

31. Ndipo Hezekia akajibu, akasema, Sasa mmejifanya wakfu kwa BWANA, karibuni mkalete dhabihu na matoleo ya shukrani nyumbani mwa BWANA. Basi kusanyiko wakaleta dhabihu na matoleo ya shukrani; na wote wenye moyo wa ukarimu, wakaleta sadaka za kuteketezwa.

32. Na hesabu ya sadaka hizo za kuteketezwa walizozileta kusanyiko ikawa ng’ombe waume sabini, kondoo waume mia, na wana-kondoo mia mbili; hao wote walikuwa ni sadaka ya kuteketezwa kwa BWANA.

2 Nya. 29