2. Yuda huomboleza,Na malango yake yamelegea;Wameketi chini wamevaa kaniki;Na kilio cha Yerusalemu kimepaa juu.
3. Na wakuu wao huwatuma watoto wao kwenye maji;Nao hufika visimani wasione maji;Hurudi, na vyombo vyao ni vitupu;Wametahayarika na kufadhaika,Na kuvifunika vichwa vyao.
4. Kwa sababu ya nchi iliyopasuka,Kwa kuwa mvua haikunyesha katika nchi,Wenye kulima wametahayarika,Na kuvifunika vichwa vyao.
5. Naam, kulungu naye uwandani amezaa,Akamwacha mwanawe kwa kuwa hapana majani.
6. Na punda-mwitu husimama juu ya vilele vya milima,Hutwetea pumzi kama mbwa-mwitu;Macho yao hayaoni sawasawa,Kwa kuwa hapana majani.
7. Ijapokuwa maovu yetu yanatushuhudia, lakini utende wewe kwa ajili ya jina lako, Ee BWANA, maana kurudi nyuma kwetu ni kwingi; tumekutenda dhambi.
8. Wewe uliye tumaini la Israeli, wewe uliye Mwokozi wake wakati wa taabu, kwa nini wewe umekuwa kama mtu akaaye katika nchi, hali ya mgeni, na kama mtu mwenye kusafiri, ageukaye upande ili kukaa usiku mmoja tu?
9. Kwa nini wewe umekuwa kama mtu aliyesituka, kama shujaa asiyeweza kuokoa? Lakini wewe, BWANA, u katikati yetu, nasi tunaitwa kwa jina lako; usituache.
10. BWANA awaambia watu hawa hivi, Hivyo ndivyo walivyopenda kutanga-tanga; hawakuizuia miguu yao; basi, BWANA hawakubali; sasa ataukumbuka uovu wao, atawapatiliza dhambi zao.
11. Naye BWANA akaniambia, Usiwaombee watu hawa wapate heri.
12. Wafungapo, mimi sitasikia kilio chao; na watoapo sadaka za kuteketezwa na sadaka ya unga, sitazitakabali; bali nitawaangamiza kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni.
13. Ndipo nikasema, Aa, Bwana, MUNGU! Tazama, manabii huwaambia, Hamtauona upanga, wala hamtakuwa na njaa; bali nitawapa amani iliyo thabiti mahali hapa.
14. Ndipo BWANA akaniambia, Hao manabii wanatabiri uongo kwa jina langu mimi; mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao; wanawapeni unabii wa maono ya uongo, na uaguzi, na neno la ubatili, na hadaa ya mioyo yao.
15. Basi, kwa hiyo BWANA asema hivi, Kwa habari za manabii wanaotabiri kwa jina langu, wala mimi sikuwatuma, lakini husema, Upanga na njaa havitaingia katika nchi hii; Kwa upanga na njaa manabii hao wataangamizwa.
16. Na watu hao, waliopewa unabii na wao, watatupwa nje katika njia kuu za Yerusalemu kwa sababu ya upanga na njaa; wala hawatakuwa na mtu wa kuwazika, wao na wake zao, na wana wao, na binti zao; maana nitamwaga uovu wao wenyewe juu yao.