2. Tazama, Bwana ana mmoja aliye hodari, mwenye nguvu; kama dhoruba ya mvua ya mawe, tufani iharibuyo, kama dhoruba ya maji mengi yafurikayo, ndivyo atakavyotupa chini kwa mkono.
3. Taji ya kiburi ya walevi wa Efraimu itakanyagwa kwa miguu;
4. na ua la uzuri wa fahari yake linalonyauka, lililo kichwani mwa bonde linalositawi, litakuwa kama tini iliyotangulia kuiva kabla ya wakati wa hari, ambayo, aionapo yeye aiangaliaye, huila mara anapoishika mkononi mwake.
5. Katika siku ile BWANA wa majeshi atakuwa ni taji ya fahari, na kilemba cha uzuri, kwa mabaki ya watu wake.
6. Naye atakuwa roho ya hukumu kwake yeye aketiye ili ahukumu; naye atakuwa nguvu kwao wageuzao nyuma vita langoni.
7. Lakini hawa nao wamekosa kwa divai, wamepotea kwa kileo; kuhani na nabii wamekosa kwa kileo, wamemezwa kwa divai, wamepotea kwa kileo; hukosa katika maono, hujikwaa katika hukumu.
8. Maana meza zote zimejaa matapiko na uchafu, hapana mahali palipo safi.
9. Atamfundisha nani maarifa? Atamfahamisha nani habari hii? Je! Ni wale walioachishwa maziwa, walioondolewa matitini?
10. Kwa maana ni amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo.
11. La, bali kwa midomo ya watu wageni, na kwa lugha nyingine atasema na watu hawa;
12. ambao aliwaambia, Hii ndiyo raha yenu, mpeni raha yeye aliyechoka; huku ndiko kuburudika; lakini hawakutaka kusikia.
13. Kwa sababu hiyo neno la BWANA kwao litakuwa hivi, amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo; ili waende na kuanguka nyuma, na kuvunjwa, na kunaswa, na kuchukuliwa.
14. Basi, lisikieni neno la BWANA, enyi watu wenye dharau, mnaowatawala watu hawa walio ndani ya Yerusalemu.
15. Kwa sababu mmesema, Tumefanya agano na mauti, tumepatana na kuzimu; pigo lifurikalo litakapopita, halitatufikia sisi; kwa maana tumefanya maneno ya uongo kuwa kimbilio letu, tumejificha chini ya maneno yasiyo kweli;
16. kwa ajili ya hayo Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye hatafanya haraka.
17. Nami nitafanya hukumu kuwa ndiyo kanuni, na haki kuwa ndiyo timazi; na mvua ya mawe itachukulia mbali hilo kimbilio la maneno ya uongo, na maji yatapagharikisha mahali pa kujisitiri.
18. Na agano lenu mliloagana na mauti litabatilika, tena mapatano yenu mliyopatana na kuzimu hayatasimama; pigo lifurikalo litakapopita, ndipo ninyi mtakapokanyagwa nalo.
19. Kila wakati litakapopita litawachukueni. Maana litapita asubuhi baada ya asubuhi, wakati wa mchana na wakati wa usiku; na kuifahamu habari ile kutakuwa kitisho tu.
20. Maana kitanda kile ni kifupi asiweze mtu kujinyosha juu yake, na nguo ile ya kujifunika ni nyembamba asipate mtu kujizingisha.