1. Maana BWANA atamhurumia Yakobo, atamchagua Israeli tena, naye atawaweka katika nchi yao wenyewe; na mgeni atajiunga nao, nao wataambatana na nyumba ya Yakobo.
2. Na hao mataifa watawatwaa na kuwaleta mpaka mahali pao wenyewe, na nyumba ya Israeli watawamiliki, na kuwafanya watumishi na wajakazi katika nchi ya BWANA; nao watawachukua hali ya kufungwa watu wale waliowafunga wao, nao watawamiliki watu wale waliowaonea.
3. Tena itakuwa katika siku ile, ambayo BWANA atakupa raha baada ya huzuni yako, na baada ya taabu yako, na baada ya utumishi ule mgumu uliotumikishwa;
4. utatunga mithali hii juu ya mfalme wa Babeli, na kusema,Jinsi alivyokoma mwenye kuonea;Jinsi ulivyokoma mji ule wenye jeuri!
5. BWANA amelivunja gongo la wabaya,Fimbo ya enzi yao wenye kutawala.
6. Yeye aliyewapiga mataifa kwa ghadhabu,Kwa mapigo yasiyokoma;Aliyewatawala mataifa kwa hasira,Ameadhibiwa asizuie mtu.
7. Dunia yote inastarehe na kutulia;Hata huanzilisha kuimba.
8. Naam, misunobari inakufurahia,Na mierezi ya Lebanoni, ikisema,Tokea wakati ulipolazwa chini wewe,Hapana mkata miti aliyetujia.
9. Kuzimu chini kumetaharuki kwa ajili yako,Ili kukulaki utakapokuja;Huwaamsha waliokufa kwa ajili yako,Naam, walio wakuu wote wa dunia;Huwainua wafalme wote wa mataifa,Watoke katika viti vyao vya enzi.
10. Hao wote watajibu na kukuambia,Je! Wewe nawe umekuwa dhaifu kama sisi!Wewe nawe umekuwa kama sisi!
11. Fahari yako imeshushwa hata kuzimu,Na sauti ya vinanda vyako;Funza wametandazwa chini yako,Na vidudu vinakufunika.