2 Nya. 29:4-18 Swahili Union Version (SUV)

4. Akawaingiza makuhani na Walawi, akawakusanya uwandani upande wa mashariki,

5. akawaambia, Nisikieni, enyi Walawi; jitakaseni nafsi zenu sasa, mkaitakase na nyumba ya BWANA, Mungu wa baba zenu, mkautoe uchafu katika patakatifu.

6. Kwa maana baba zetu wameasi, na kufanya yaliyo maovu machoni pa BWANA, Mungu wetu, wamemwacha, na kugeuzia mbali nyuso zao na makao ya BWANA, na kumpa maungo.

7. Tena wameifunga milango ya ukumbi, na kuzizima taa, wala hawakufukiza uvumba, wala hawakumtolea Mungu wa Israeli sadaka za kuteketezwa katika patakatifu.

8. Kwa hiyo hasira ya BWANA imekuwa juu ya Yuda na Yerusalemu, naye amewatoa kuwa matetemeko, wawe ushangao, na mazomeo, kama mwonavyo kwa macho yenu.

9. Kwa kuwa, tazama, baba zetu wameangamia kwa upanga, na wana wetu, na binti zetu, na wake zetu wametekwa kwa ajili ya hayo.

10. Basi nia yangu ni kufanya agano na BWANA, Mungu wa Israeli, ili kwamba hasira yake kali itugeukie mbali.

11. Basi wanangu, msijipurukushe sasa, kwa kuwa BWANA amewachagua ninyi msimame mbele yake, kumhudumia, nanyi mpate kuwa watumishi wake, mkafukize uvumba.

12. Ndipo wakaondoka Walawi, Mahathi mwana wa Amasai, na Yoeli mwana wa Azaria, wa wana wa Wakohathi; na wa wana wa Merari, Kishi mwana wa Abdi, na Azaria mwana wa Yehaleleli; na wa Wagershoni, Yoa mwana wa Zima na Edeni mwana wa Yoa;

13. na wa wana wa Elisafani, Shimri na Yeueli; na wa wana wa Asafu, Zekaria na Matania;

14. na wa wana wa Hemani, Yehueli na Shimei; na wa wana wa Yeduthuni, Shemaya na Uzieli.

15. Wakawakusanya ndugu zao, wakajitakasa, wakaingia, kama alivyoamuru mfalme kwa maneno ya BWANA, ili waisafishe nyumba ya BWANA.

16. Nao makuhani wakaingia nyumbani mwa BWANA, katika mahali pa ndani, ili waisafishe, wakatoa uchafu wote waliouona hekaluni mwa BWANA, wakautupa nje uani mwa nyumba ya BWANA. Walawi wakautwaa, ili wauchukue nje mpaka kijito cha Kidroni.

17. Basi wakaanza kutakasa siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, hata siku ya nane ya mwezi wakafika katika ukumbi wa BWANA; wakaitakasa nyumba ya BWANA katika muda wa siku nane; wakamaliza siku ya kumi na sita ya mwezi wa kwanza.

18. Wakaingia ndani kwa Hezekia mfalme, wakasema, Tumeisafisha nyumba yote ya BWANA, na madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, pamoja na vyombo vyake vyote, na meza ya mikate ya wonyesho, pamoja na vyombo vyake vyote.

2 Nya. 29