3. Abiya akapanga vita mwenye jeshi la watu hodari wa vita, watu wateule mia nne elfu; naye Yeroboamu akapanga vita juu yake mwenye watu wateule mia nane elfu, waliokuwa waume mashujaa.
4. Basi Abiya akasimama juu ya kilima cha Semaraimu, kilichoko milimani mwa Efraimu, akasema, Nisikieni, enyi Yeroboamu na Israeli wote;
5. je! Haikuwapasa kujua ya kwamba BWANA, Mungu wa Israeli, alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele, yeye na wanawe kwa agano la chumvi?
6. Lakini Yeroboamu mwana wa Nebati, mtumwa wa Sulemani mwana wa Daudi, akainuka, akamfanyia fitina bwana wake.
7. Wakamkusanyikia watu mabaradhuli, wasiofaa kitu, waliojitia nguvu juu ya Rehoboamu mwana wa Sulemani, Rehoboamu alipokuwa kijana na wa moyo mwororo, asiweze kuwazuia.
8. Hata sasa mwajidhania kuwa mtauzuia ufalme wa BWANA mikononi mwa wana wa Daudi; nanyi mmekuwa jamii kubwa, na kwenu mna ndama za dhahabu alizowafanyia Yeroboamu kuwa miungu.
9. Je! Hamkuwafukuza makuhani wa BWANA, wana wa Haruni, na Walawi; mkajifanyia makuhani kama wafanyavyo watu wa nchi nyingine? Hata ye yote ajaye kujifanya wakfu na ndama, na kondoo waume saba, aweza kuwa kuhani wa hiyo isiyo miungu.
10. Lakini sisi, BWANA ndiye Mungu wetu, wala sisi hatukumwacha; tena tunao makuhani wanaomtumikia BWANA, wana wa Haruni, na Walawi, kwa kazi yao;
11. nao humtolea BWANA kila asubuhi, na kila jioni, sadaka za kuteketezwa na fukizo la manukato; mikate ya wonyesho pia huiweka kwa taratibu yake juu ya meza takatifu, na kinara cha dhahabu chenye taa zake, kuwaka kila jioni; kwa maana sisi twayalinda malinzi ya BWANA, Mungu wetu; bali ninyi mmemwacha.
12. Na tazama, Mungu yu pamoja nasi atutangulie, na makuhani wake wenye mapanda, ili wapige sauti ya kugutusha juu yenu. Enyi wana wa Israeli, msipigane na BWANA, Mungu wa baba zenu; kwani hamtafanikiwa.
13. Lakini Yeroboamu aliwazungushia waviziao kwa nyuma; basi wao wakawa mbele ya Yuda, na wale waviziao nyuma yao.
14. Na Yuda walipotazama nyuma, angalia, vita vikawa mbele na nyuma; wakamlilia BWANA, na makuhani wakapiga mapanda.