1 Sam. 20:8-23 Swahili Union Version (SUV)

8. Basi, unitendee mema mimi mtumishi wako; kwa sababu umenitia mimi mtumishi wako katika agano la BWANA pamoja nawe, lakini ikiwa mna uovu moyoni mwangu, uniue wewe mwenyewe; kwa nini kunileta kwa baba yako?

9. Naye Yonathani akasema, Haya na yawe mbali nawe, kwa maana kama ningejua ya kuwa baba yangu amekusudia kukutenda neno baya, je! Singekuambia?

10. Basi Daudi akamwambia Yonathani, Ni nani atakayeniambia, ikiwa baba yako amekujibu maneno makali?

11. Yonathani akamwambia Daudi, Twende zetu nje mashambani. Wakatoka wote wawili, wakaenda mashambani.

12. Naye Yonathani akamwambia Daudi, BWANA, Mungu wa Israeli, na awe shahidi; nitakapokuwa nimekwisha kumwuliza baba yangu, kama wakati huu kesho, au siku ya tatu, angalia, kama liko neno jema la kumfaa Daudi, je! Nisikupelekee habari na kukufunulia neno hili?

13. BWANA anitende mimi, Yonathani, hivyo, na kuzidi, ikiwa yampendeza babangu kukutenda mabaya, nisipokufunulia haya, na kukupeleka uende zako kwa amani; na BWANA awe pamoja nawe, kama alivyokuwa pamoja na baba yangu.

14. Nawe utanionyesha fadhili za BWANA, ili nisife, si wakati huu tu maadamu mimi ni hai;

15. lakini pamoja na hayo, hata jamaa yangu pia hutawaondolea kabisa fadhili zako; la, hata wakati ule BWANA atakapokuwa amewaondoa kabisa adui za Daudi wote pia katika uso wa nchi.

16. Basi Yonathani akafanya agano na jamaa yake Daudi, akisema, BWANA naye atayataka mkononi mwa adui zake Daudi.

17. Naye Yonathani akamwapisha Daudi mara ya pili, kwa ajili ya upendo aliokuwa nao kwake; kwa maana alimpenda kama alivyoipenda roho yake mwenyewe.

18. Kisha Yonathani akamwambia, Kesho ni mwandamo wa mwezi, nawe utakosekana, kwa sababu kiti chako kitakuwa hakina mtu.

19. Nawe ukiisha kungoja siku tatu, shuka upesi ufike kuko huko ulikojificha, siku ya shughuli ile; nawe kaa karibu na kile kichuguu kule.

20. Nami nitapiga mishale mitatu kando-kando yake, kana kwamba ninapiga shabaha.

21. Kisha, angalia, nitamtuma mtoto na kumwambia, Nenda ukaitafute mishale. Hapo nikimwambia yule mtoto, Tazama, mishale iko upande wako huu, itwae; basi uje, maana iko amani kwako, wala hapana hatari, BWANA aishivyo.

22. Bali nikimwambia yule mtoto, Tazama, mishale iko huko mbele yako; basi enenda zako, kwa maana BWANA amekuamuru uende zako.

23. Na kwa habari ya neno lile tulilonena, wewe na mimi, angalia BWANA yu kati ya wewe na mimi milele.

1 Sam. 20