Zab. 77:1-12 Swahili Union Version (SUV)

1. Nimpazie Mungu sauti yangu,Naam, nimpazie Mungu, naye atanisikia.

2. Siku ya taabu yangu nalimtafuta Bwana;Mkono wangu ulinyoshwa usiku, haukulegea;Nafsi yangu ilikataa kufarijika.

3. Nilipotaka kumkumbuka Mungu nalifadhaika;Nilipotaka kutafakari roho yangu ilizimia.

4. Ulizishika kope za macho yangu zisifumbike;Naliona mashaka nisiweze kunena.

5. Nalifikiri habari za siku za kale,Miaka ya zamani zilizopita.

6. Nakumbuka wimbo wangu usiku,Nawaza moyoni mwangu,Roho yangu ikatafuta.

7. Je! Bwana atatupa milele na milele?Hatatenda fadhili tena kabisa?

8. Rehema zake zimekoma hata milele?Ahadi yake imekwisha hata vizazi vyote?

9. Mungu amesahau fadhili zake?Amezuia kwa hasira rehema zake?

10. Nikasema, Ndio udhaifu wangu huo;Lakini nitaikumbuka miaka ya mkono wa kuume wake Aliye juu.

11. Nitayakumbuka matendo ya BWANA;Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale.

12. Pia nitaitafakari kazi yako yote;Nitaziwaza habari za matendo yako.

Zab. 77