10. Ndipo mfalme wa Babeli akawaua wana wa Sedekia mbele ya macho yake; pia akawaua wakuu wote wa Yuda huko Ribla.
11. Akampofusha macho Sedekia; tena mfalme wa Babeli akamfunga kwa pingu, akamchukua mpaka Babeli, akamtia gerezani hata siku ya kufa kwake.
12. Basi katika mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi, ndio mwaka wa kumi na kenda wa mfalme Nebukadreza, mfalme wa Babeli; Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, aliyesimama mbele ya mfalme wa Babeli, aliingia Yerusalemu.
13. Akaiteketeza nyumba ya BWANA, na nyumba ya mfalme; na nyumba zote za Yerusalemu, naam, kila nyumba kubwa aliiteketeza kwa moto.
14. Na jeshi lote la Wakaldayo, waliokuwa pamoja na huyo amiri wa askari walinzi, wakazibomoa kuta zote za Yerusalemu pande zote.
15. Kisha Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua wafungwa baadhi ya watu waliokuwa maskini, na mabaki ya watu walioachwa katika mji, nao wale walioasi na kumkimbilia mfalme wa Babeli, nao mabaki ya vibarua.
16. Lakini Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawaacha watu walio maskini kabisa ili wawe watunza mizabibu na wakulima.
17. Na nguzo za shaba zilizokuwa katika nyumba ya BWANA, na matako ya bahari ya shaba iliyokuwa katika nyumba ya BWANA, Wakaldayo walivivunja vipande vipande, wakaichukua shaba yake yote mpaka Babeli.
18. Nayo masufuria, na majembe, na makasi, na mabakuli, na miiko, na vyombo vyote vya shaba walivyokuwa wakivitumia, wakavichukua vyote.
19. Navyo vikombe, na vyombo vya kutolea majivu, na mabakuli, na masufuria, na vinara, na miiko, na vyetezo, vilivyokuwa vya dhahabu katika dhahabu, na vilivyokuwa vya fedha katika fedha, amiri wa askari walinzi akavichukua.
20. Nguzo mbili, bahari moja, na ng’ombe kumi na mbili za shaba zilizokuwa chini ya matako yake, ambavyo mfalme Sulemani aliifanyia nyumba ya BWANA; shaba ya vitu hivyo vyote ilikuwa haiwezi kupimwa kwa kuwa nyingi sana.
21. Na nguzo hizo, urefu wa nguzo moja ulikuwa dhiraa kumi na nane, na uzi wa dhiraa kumi na mbili ungeweza kuizunguka; na unene wake ulikuwa nyanda nne; nayo ilikuwa ya uvungu.
22. Nayo ilikuwa na kichwa cha shaba juu yake; na urefu wa kichwa kimoja ulikuwa dhiraa tano; palikuwa na mapambo ya wavu na makomamanga juu ya kichwa hicho pande zote; vyote vilikuwa vya shaba; nayo nguzo ya pili ilikuwa na mapambo kama hayo, na makomamanga.
23. Palikuwa na makomamanga tisini na sita katika pande zake; makomamanga; yote yalikuwa mia juu ya wavu huo pande zote.
24. Naye amiri wa askari walinzi akamtwaa Seraya, kuhani mkuu, na Sefania, kuhani wa pili, na wale walinzi watatu wa mlango;
25. na katika mji akatwaa towashi mmoja aliyewasimamia watu wa vita; na watu saba katika wale waliouona uso wa mfalme, walioonekana katika mji; na karani wa jemadari wa jeshi, aliyewaandika watu wa nchi; na watu sitini katika watu wa nchi, walioonekana ndani ya mji.