Mwa. 4:16-26 Swahili Union Version (SUV)

16. Kaini akatoka mbele za uso wa BWANA, akakaa katika nchi ya Nodi, mbele ya Edeni.

17. Kaini akamjua mkewe; naye akapata mimba, akamzaa Henoko; akajenga mji akauita Henoko, kwa jina la mwanawe.

18. Henoko akamzaa Iradi, Iradi akamzaa Mehuyaeli; Mehuyaeli akamzaa Methushaeli; Methushaeli akamzaa Lameki.

19. Lameki akajitwalia wake wawili, jina la wa kwanza ni Ada, na jina la wa pili ni Sila.

20. Ada akamzaa Yabali; huyo ndiye baba yao wakaao katika hema na kufuga wanyama.

21. Na jina la nduguye aliitwa Yubali; huyo ndiye baba yao wapigao kinubi na filimbi.

22. Sila naye akamzaa Tubal-kaini, mfua kila chombo cha kukatia, cha shaba na cha chuma; na umbu lake Tubal-kaini alikuwa Naama.

23. Lameki akawaambia wake zake,Sikieni sauti yangu, Ada na Sila;Enyi wake za Lameki, sikilizeni usemi wangu;Maana nimemwua mtu kwa kunitia jeraha;Kijana kwa kunichubua;

24. Kama Kaini akilipiwa kisasi mara saba,Hakika Lameki atalipiwa mara sabini na saba.

25. Adamu akamjua mke wake tena; akazaa mwana mwanamume, akamwita jina lake Sethi; maana alisema, Mungu ameniwekea uzao mwingine mahali pa Habili; kwa sababu Kaini alimwua.

26. Sethi naye akazaa mwana; akamwita jina lake Enoshi. Hapo ndipo watu walipoanza kuliitia Jina la BWANA.

Mwa. 4