14. Akaenda, akawatwaa, akamletea mamaye. Mamaye akafanya chakula kitamu namna ile aliyopenda babaye.
15. Kisha Rebeka akatwaa mavazi mazuri ya Esau mwanawe mkubwa, aliyokuwa nayo nyumbani, akamvika Yakobo mwanawe mdogo.
16. Na ngozi za wana-mbuzi akamvika mikononi, na katika ulaini wa shingo yake.
17. Naye akampa Yakobo mwanawe mikononi mwake hicho chakula kitamu, na mkate alioufanya.
18. Akaja kwa baba yake, akasema, Babangu. Akasema, Mimi hapa, U nani wewe, mwanangu?
19. Yakobo akamwambia babaye, Mimi ni Esau, mzaliwa wako wa kwanza, nimefanya kama ulivyoniambia. Ondoka, tafadhali, ukae kitako, ule mawindo yangu, ili roho yako inibariki.
20. Isaka akamwuliza mwanawe, Imekuwaje umepata upesi namna hii, mwanangu? Akasema, Kwa sababu BWANA, Mungu wako, amenifanikisha.
21. Isaka akamwambia Yakobo, Karibu, tafadhali, ili nikupapase, mwanangu, nione kwamba wewe ndiwe mwanangu Esau, ama siyo.
22. Basi Yakobo akamkaribia Isaka, babaye, naye akampapasa, akasema, Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.
23. Wala hakumtambua, kwa maana mikono yake ilikuwa kama mikono ya Esau, ndugu yake, yenye malaika; basi akambariki.
24. Akamwuliza, Wewe ndiwe kweli mwanangu Esau? Akasema, Ndimi.
25. Akasema, Niletee karibu nami nipate kula mawindo ya mwanangu, ili roho yangu ikubariki. Akamsogezea karibu, naye akala; kisha akamletea mvinyo, akanywa.
26. Isaka, baba yake, akamwambia, Njoo karibu sasa, ukanibusu, mwanangu.
27. Akakaribia akambusu. Naye akasikia harufu ya mavazi yake, akambariki akasema,Tazama, harufu ya mwananguNi kama harufu ya shamba alilolibariki Bwana.
28. Mungu na akupe ya umande wa mbingu,Na ya manono ya nchi,Na wingi wa nafaka na mvinyo.