15. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito,Na kwa masikio yao hawasikii vema,Na macho yao wameyafumba;Wasije wakaona kwa macho yao,Wakasikia kwa masikio yao,Wakaelewa kwa mioyo yao,Wakaongoka, nikawaponya.
16. Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia.
17. Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie.
18. Basi ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi.
19. Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia.
20. Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha;
21. lakini hana mizizi ndani yake, bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa.
22. Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai.
23. Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini.
24. Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake;
25. lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake.
26. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu.
27. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu?
28. Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye?
29. Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo.