13. Lakini nawaambia, Eliya amekwisha kuja, nao wakamtenda yote waliyoyataka kama alivyoandikiwa.
14. Hata walipowafikia wanafunzi, waliona mkutano mkuu wakiwazunguka, na waandishi wakijadiliana nao;
15. mara mkutano wote walipomwona walishangaa, wakamwendea mbio, wakamsalimu.
16. Akawauliza, Mnajadiliana nini nao?
17. Mtu mmoja katika mkutano akamjibu, Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo bubu;
18. na kila ampagaapo, humbwaga chini, naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda; nikasema na wanafunzi wako wamtoe pepo, wasiweze.
19. Akawajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu.
20. Wakamleta kwake; hata alipomwona, mara yule pepo alimtia kifafa; naye akaanguka chini, akagaa-gaa, akitokwa na povu.
21. Akamwuliza babaye, Amepatwa na haya tangu lini? Akasema, Tangu utoto.
22. Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia.
23. Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye.
24. Mara babaye yule kijana akapaza sauti, akasema, Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu.