Mit. 31:1-17 Swahili Union Version (SUV)

1. Maneno ya mfalme Lemueli; mausia aliyofundishwa na mama yake.

2. Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu?Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu?

3. Usiwape wanawake nguvu zako;Wala moyo wako usiwape wale wawaharibuo wafalme.

4. Ee Lemueli, kunywa mvinyo hakuwafai wafalme, hakuwafai wafalme;Wala haifai wakuu waseme, Ki wapi kileo?

5. Wasije wakanywa na kuisahau sheria,Na kuipotosha hukumu ya mtu aliye taabuni.

6. Mpe kileo yeye aliye karibu na kupotea;Kampe divai yeye aliye na uchungu nafsini.

7. Anywe akausahau umaskini wake;Asiikumbuke tena taabu yake.

8. Fumbua kinywa chako kwa ajili yake aliye bubu;Uwatetee watu wote walioachwa peke yao;

9. Fumbua kinywa chako, uhukumu kwa haki;Uwapatie maskini na wahitaji haki yao.

10. Mke mwema, ni nani awezaye kumwona?Maana kima chake chapita kima cha marijani.

11. Moyo wa mumewe humwamini,Wala hatakosa kupata mapato.

12. Humtendea mema wala si mabaya,Siku zote za maisha yake.

13. Hutafuta sufu na kitani;Hufanya kazi yake ya mikono kwa moyo.

14. Afanana na merikebu za biashara;Huleta chakula chake kutoka mbali.

15. Tena huamka, kabla haujaisha usiku;Huwapa watu wa nyumbani mwake chakula;Na wajakazi wake sehemu zao.

16. Huangalia shamba, akalinunua;Kwa mapato ya mikono yake hupanda mizabibu.

17. Hujifunga nguvu viunoni kama mshipi;Hutia mikono yake nguvu.

Mit. 31