Mit. 14:6-18 Swahili Union Version (SUV)

6. Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate;Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu.

7. Toka mbele ya uso wa mpumbavu,Maana hutaona kwake midomo ya maarifa.

8. Akili za mwenye busara ni kujua njia yake;Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu.

9. Wapumbavu huidharau hatia;Bali upo upendeleo kwa wenye haki.

10. Moyo huujua uchungu wa nafsi yake,Wala mgeni haishiriki furaha yake.

11. Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa;Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa.

12. Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu,Lakini mwisho wake ni njia za mauti.

13. Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni;Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo.

14. Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe;Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake.

15. Mjinga huamini kila neno;Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.

16. Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu;Bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai.

17. Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga;Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa.

18. Wajinga hurithi upumbavu;Bali wenye busara huvikwa taji ya maarifa.

Mit. 14