Mhu. 12:1-10 Swahili Union Version (SUV)

1. Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako,Kabla hazijaja siku zilizo mbaya,Wala haijakaribia miaka utakaposema,Mimi sina furaha katika hiyo.

2. Kabla jua, na nuru, na mwezi,Na nyota, havijatiwa giza;Kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua;

3. Siku ile walinzi wa nyumba watakapotetema;Hapo wenye nguvu watakapojiinamisha;Na wasagao kukoma kwa kuwa ni haba;Na hao wachunguliao madirishani kutiwa giza;

4. Na milango kufungwa katika njia kuu;Sauti ya kinu itakapokuwa ni ndogo;Na mtu kusituka kwa sauti ya ndege;Nao binti za kuimba watapunguzwa;

5. Naam, wataogopa kilichoinukaNa vitisho vitakuwapo njiani;Na mlozi utachanua maua;Na panzi atakuwa ni mzigo mzito;Na pilipili hoho itapasuka;Maana mtu aiendea nyumba yake ya milele,Nao waombolezao wazunguka njiani.

6. Kabla haijakatika kamba ya fedha;Au kuvunjwa bakuli la dhahabu;Au mtungi kuvunjika kisimani;Au gurudumu kuvunjika birikani;

7. Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa,Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.

8. Mhubiri asema, Ubatili mtupu; mambo yote ni ubatili!

9. Walakini, kwa sababu huyo Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa, naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi.

10. Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.

Mhu. 12