Kut. 40:12-25 Swahili Union Version (SUV)

12. Kisha utamleta Haruni na wanawe hapo mlangoni pa hema ya kukutania, nawe utawaosha kwa maji.

13. Kisha utamvika Haruni mavazi matakatifu; nawe utamtia mafuta, na kumweka awe mtakatifu, ili apate kunitumikia katika kazi ya ukuhani.

14. Kisha utawaleta wanawe, na kuwavika kanzu zao;

15. nawe utawatia mafuta kama ulivyomtia mafuta baba yao, ili wanitumikie katika kazi ya ukuhani; na huko kutiwa mafuta kwao kutakuwa ni kwa ukuhani wa milele katika vizazi vyao vyote.

16. Musa akafanya hayo yote; kama yote BWANA aliyoagiza ndivyo alivyofanya.

17. Hata mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili, siku ya kwanza ya mwezi ile maskani ilisimamishwa.

18. Musa akaisimamisha maskani, akayaweka matako yake, akazisimamisha mbao zake akayatia mataruma yake, akazisimamisha nguzo zake.

19. Akaitanda hema juu ya maskani, akakitia kifuniko cha hema juu yake; kama BWANA alivyomwamuru Musa.

20. Akautwaa ule ushuhuda, akautia ndani ya sanduku, akaiweka miti ya kuchukulia juu ya sanduku, akakiweka kiti cha rehema juu ya sanduku;

21. kisha akalileta sanduku akalitia ndani ya maskani, naye akalitundika pazia la sitara, akalisitiri sanduku la ushuhuda; kama BWANA alivyomwamuru Musa.

22. Akaitia meza ndani ya hema ya kukutania, upande wa maskani ulioelekea kaskazini, nje ya pazia.

23. Akaipanga ile mikate juu yake mbele za BWANA; kama BWANA alivyomwamuru Musa.

24. Kisha akakitia kinara cha taa ndani ya hema ya kukutania, kuikabili ile meza, upande wa maskani ulioelekea kusini.

25. Kisha akaziwasha taa zake mbele za BWANA, kama BWANA alivyomwamuru Musa.

Kut. 40