Kum. 2:7-26 Swahili Union Version (SUV)

7. Kwa kuwa BWANA, Mungu wako, amekubarikia katika kazi yote ya mkono wako; amejua ulivyotembea katika jangwa kubwa hili; miaka arobaini hii alikuwa nawe BWANA, Mungu wako; hukukosa kitu.

8. Basi tukapita kando yao ndugu zetu wana wa Esau, waketio Seiri kutoka njia ya Araba, kutoka Elathi na kutoka Esion-geberi.Tukageuka tukapita njia ya bara ya Moabu.

9. BWANA akaniambia, usiwasumbue Wamoabi, wala usishindane nao katika mapigano; kwa kuwa sitakupa katika nchi yake kuimiliki; kwa sababu Ari nimewapa wana wa Lutu kuimiliki.

10. (Walioketi humo hapo kale ni Waemi, nao ni watu wakubwa, wengi, warefu, mfano wa Waanaki;

11. na hawa nao wadhaniwa kuwa majitu kama Waanaki; lakini Wamoabi huwaita Waemi.

12. Na Wahori nao walikuwa wakikaa Seiri hapo kale, lakini wana wa Esau waliwafuata; wakawaangamiza mbele yao, wakakaa badala yao; kama alivyofanya Israeli nchi ya milki yake aliyopewa na BWANA.)

13. Sasa basi ondokeni, mkakivuke kijito cha Zeredi. Nasi tukakivuka kile kijito cha Zeredi.

14. Na siku tulizokuwa tukienda kutoka Kadesh-barnea hata tulipovuka kijito cha Zeredi, zilikuwa ni miaka thelathini na minane; maana, hata walipokwisha kuangamizwa watu wa vita kutoka kati ya marago, kizazi chao chote, kama walivyoapiwa na BWANA.

15. Tena mkono wa BWANA ulikuwa juu yao ili kuwaangamiza, kuwatoa kati ya marago, hata walipokoma.

16. Basi ikawa, walipokwisha angamizwa kwa kufa watu wote wa vita kati ya watu,

17. BWANA aliniambia, akasema,

18. Hivi leo ivuke Ari, mpaka wa Moabu;

19. na utakaposongea kuwaelekea wana wa Amoni, usiwasumbue wana wa Amoni, wala usishindane nao; kwa kuwa sitakupa katika nchi ya hao wana wa Amoni kuwa milki yako; kwa sababu nimewapa wana wa Lutu iwe milki yao.

20. (Nchi hiyo nayo yadhaniwa kuwa ni nchi ya Warefai, hapo kale Warefai walikaa humo; lakini Waamoni huwaita Wazamzumi;

21. nao ni watu wengi, wakubwa, warefu, kama Waanaki; lakini BWANA aliwaangamiza mbele yao; wakawafuata wakakaa badala yao;

22. kama vile alivyowafanyia wana wa Esau, waliokaa Seiri, alipowaangamiza Wahori mbele yao; wakawafuata, wakakaa badala yao hata hivi leo;

23. na Waavi waliokuwa wakikaa katika vijiji mpaka Gaza waliangamizwa na Wakaftori waliotoka Kaftori, na hawa wakakaa badala yao.)

24. Ondokeni, mshike safari yenu, mvuke bonde la Arnoni; tazama, nimemtia Sihoni Mwamori mfalme wa Heshboni mkononi mwako, na nchi yake; anzeni kuimiliki, mshindane naye katika mapigano.

25. Hivi leo nitaanza mimi kutia utisho wako na kuhofiwa kwako juu ya watu walio chini ya mbingu kila mahali, watakaosikia uvumi wako, na kutetemeka, na kuingiwa na uchungu kwa sababu yako.

26. Nikatuma wajumbe kutoka bara ya Kedemothi kwenda kwa Sihoni mfalme wa Heshboni na maneno ya amani, kusema.

Kum. 2