18. Akamwambia, Mimi nami ni nabii kama wewe, na malaika akaniambia kwa neno la BWANA, kusema, Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako, ale chakula, akanywe maji. Lakini alisema uongo.
19. Basi mtu yule akarudi pamoja naye, akala chakula, akanywa maji nyumbani mwake.
20. Hata ikawa, walipokuwa wameketi mezani, neno la BWANA likamjia nabii yule aliyemrudisha;
21. akamlilia yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda, akinena, BWANA asema hivi, Kwa sababu umeiasi kauli ya BWANA, wala hukuishika amri ile aliyokuamuru BWANA, Mungu wako,
22. bali umerudi, ukala chakula ukanywa maji, hapo alipokuambia, Usile chakula, wala usinywe maji; maiti yako haitaliingia kaburi la baba zako.
23. Basi ikawa, alipokwisha kula chakula na kunywa maji, yule nabii aliyemrudisha akamtandikia punda.
24. Na alipokuwa amekwenda zake, simba alimkuta njiani, akamwua. Maiti yake ikatupwa njiani, na yule punda akasimama karibu naye; na yule simba naye akasimama karibu na maiti.
25. Na tazama, watu wakapita, wakauona mzoga umetupwa njiani, na yule simba akisimama karibu na mzoga, wakaenda, wakatoa habari katika mji ule alimokaa yule nabii mzee.
26. Na yule nabii aliyemrudisha njiani alipopata habari, akasema; Ndiye yule mtu wa Mungu, aliyeiasi kauli ya BWANA; kwa hiyo BWANA amempambanisha na simba, simba akamrarua, akamwua, sawasawa na neno la BWANA alilomwambia.