20. Lakini nyinyi ndio watu aliowakomboa kutoka Misri katika tanuri la chuma. Aliwatoeni huko ili muwe watu wake kama vile mlivyo hivi leo.
21. Kwa sababu yenu Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alinikasirikia, akaapa kwamba mimi sitavuka mto Yordani kuingia katika nchi ile nzuri anayowapeni iwe mali yenu.
22. Mimi nitafia katika nchi hii wala sitauvuka mto, lakini nyinyi mko karibu kuuvuka na kwenda kuimiliki nchi ile nzuri.
23. Jihadharini sana msije mkasahau agano ambalo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amefanya nanyi; msijifanyie sanamu ya kuchonga katika umbo la kitu chochote ambacho Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amewakataza kumfananisha,
24. maana Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ni moto uteketezao; yeye ni Mungu mwenye wivu.