Zab. 119:131-141 Swahili Union Version (SUV)

131. Nalifunua kinywa changu nikatweta,Maana naliyatamani maagizo yako.

132. Unigeukie, unirehemu mimi,Kama iwahusuvyo walipendao jina lako.

133. Uzielekeze hatua zangu kwa neno lako,Uovu usije ukanimiliki.

134. Unikomboe na dhuluma ya mwanadamu,Nipate kuyashika mausia yako.

135. Umwangazie mtumishi wako uso wako,Na kunifundisha amri zako.

136. Macho yangu yachuruzika mito ya maji,Kwa sababu hawaitii sheria yako.

137. Ee BWANA, Wewe ndiwe mwenye haki,Na hukumu zako ni za adili.

138. Umeziagiza shuhuda zako kwa haki,Na kwa uaminifu mwingi.

139. Juhudi yangu imeniangamiza,Maana watesi wangu wameyasahau maneno yako.

140. Neno lako limesafika sana,Kwa hiyo mtumishi wako amelipenda.

141. Mimi ni mdogo, nadharauliwa,Lakini siyasahau mausia yako.

Zab. 119