Yer. 23:22-34 Swahili Union Version (SUV)

22. Lakini kama wangalisimama katika baraza yangu, ndipo wangaliwasikizisha watu wangu maneno yangu, na kuwageuza waziache njia zao mbaya, na uovu wa matendo yao.

23. Mimi ni Mungu aliye karibu, asema BWANA, mimi si Mungu aliye mbali.

24. Je, mtu ye yote aweza kujificha mahali pa siri, nisimwone? Asema BWANA. Je! Mbingu na nchi hazikujawa nami? Asema BWANA.

25. Nimesikia waliyoyasema manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, Nimeota ndoto; nimeota ndoto.

26. Je! Mambo hayo yatakuwa katika mioyo ya manabii wanaotabiri uongo hata lini, manabii hao wenye udanganyifu katika mioyo yao wenyewe?

27. Wanaodhania ya kuwa watawasahaulisha watu wangu jina langu kwa ndoto zao, wanazomhadithia kila mtu jirani yake, kama vile baba zao walivyolisahau jina langu, kwa ajili ya Baali.

28. Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema BWANA.

29. Je! Neno langu si kama moto? Asema BWANA; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?

30. Basi kwa sababu hiyo mimi ni juu ya manabii hao, asema BWANA, wanaompokonya kila mtu jirani yake maneno yangu.

31. Tazama, mimi ni juu ya manabii, asema BWANA, wanaotumia ndimi zao na kusema, Yeye asema,

32. Tazama, mimi ni juu ya hao wanaotabiri ndoto za uongo, asema BWANA, na kuzisema, na kuwakosesha watu wangu kwa uongo wao, na kwa majivuno yao ya upuzi, lakini mimi sikuwatuma, wala sikuwapa amri; wala hawatawafaidia watu hawa hata kidogo, asema BWANA.

33. Na watu hawa, au nabii au kuhani, atakapokuuliza, akisema, Mzigo wa BWANA ni nini? Ndipo utawaambia, Mzigo gani? BWANA asema, Nitawatupilia mbali.

34. Na katika habari ya nabii, na kuhani, na watu, watakaosema, Mzigo wa BWANA, mimi nitamwadhibu mtu yule, na nyumba yake.

Yer. 23