11. Naye Naomi akasema, Enyi wanangu, mrejee; kwani kufuatana na mimi? Je! Mimi ninao watoto wa kiume tena tumboni mwangu, hata wawe waume zenu?
12. Enyi wanangu, mrejee; nendeni zenu; kwa kuwa mimi ni mzee, siwezi kupata mume tena. Kama ningesema, Natumaini; kama ningepata mume hata usiku huu, na kuzaa watoto wa kiume;
13. je! Mngesubiri hata watakapokuwa watu wazima? Mngejizuia msiwe na waume? La, sivyo, wanangu; maana ni vigumu kwangu kuliko kwenu, kwa sababu mkono wa BWANA umetoka juu yangu.
14. Nao wakapaza sauti zao, wakalia tena, na Orpa akambusu mkwewe, lakini Ruthu akaambatana naye.
15. Naye akasema, Tazama, shemeji yako amerejea kwa watu wake, na kwa mungu wake; basi urejee wewe umfuate shemeji yako.
16. Naye Ruthu akasema,Usinisihi nikuache,Nirejee nisifuatane nawe;Maana wewe uendako nitakwenda,Na wewe ukaapo nitakaa.Watu wako watakuwa watu wangu,Na Mungu wako atakuwa Mungu wangu;
17. Pale utakapokufa nitakufa nami,Na papo hapo nitazikwa;BWANA anitende vivyo na kuzidi,Ila kufa tu kutatutenga wewe nami.
18. Basi alipomwona kuwa amekaza nia yake kufuatana naye, aliacha kusema naye.
19. Hivyo hao wakaendelea wote wawili hata walipofika Bethlehemu. Na ikawa walipofika Bethlehemu, mji wote ulitaharuki kwa habari zao. Nao wanawake wakasema, Je! Huyu ni Naomi?
20. Akawaambia, Msiniite Naomi, niiteni Mara, kwa sababu Mwenyezi Mungu amenitenda mambo machungu sana.
21. Mimi nalitoka hali nimejaa, naye BWANA amenirudisha sina kitu, kwani kuniita Naomi, ikiwa BWANA ameshuhudia juu yangu, na Mwenyezi Mungu amenitesa?
22. Basi Naomi akarudi; pamoja na Ruthu Mmoabi, mkwewe; ambao walirudi kutoka nchi ya Moabu; nao wakafika Bethlehemu mwanzo wa mavuno ya shayiri.