Omb. 5 Swahili Union Version (SUV)

Ombi la Kuhurumiwa

1. Ee BWANA, kumbuka yaliyotupata;Utazame na kuiona aibu yetu.

2. Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni;Na nyumba zetu kuwa mali ya makafiri.

3. Tumekuwa yatima waliofiwa na baba;Mama zetu wamekuwa kama wajane.

4. Tumekunywa maji yetu kwa fedha;Kuni zetu twauziwa.

5. Watufuatiao wa juu ya shingo zetu;Tumechoka tusipate raha yo yote.

6. Tumewapa hao Wamisri mkono;Na Waashuri nao, ili tushibe chakula.

7. Baba zetu walitenda dhambi hata hawako;Na sisi tumeyachukua maovu yao.

8. Watumwa wanatutawala;Hakuna mtu wa kutuokoa na mikono yao.

9. Twapata chakula kwa kujihatarisha nafsi zetu;Kwa sababu ya upanga wa nyikani.

10. Ngozi yetu ni nyeusi kama tanuu;Kwa sababu ya hari ya njaa ituteketezayo.

11. Huwatia jeuri wanawake katika Sayuni;Na mabikira katika miji ya Yuda.

12. Wakuu hutungikwa kwa mikono yao;Nyuso za wazee hazipewi heshima.

13. Vijana huyachukua mawe ya kusagia;Na watoto hujikwaa chini ya kuni.

14. Wazee wameacha kwenda langoni;Na vijana kwenda ngomani.

15. Furaha ya mioyo yetu imekoma;Machezo yetu yamegeuka maombolezo.

16. Taji ya kichwa chetu imeanguka;Ole wetu! Kwa kuwa tumetenda dhambi.

17. Kwa sababu hiyo mioyo yetu imezimia;Kwa ajili ya hayo macho yetu hayaoni vema.

18. Kwa ajili ya mlima Sayuni ulio ukiwa,Mbweha hutembea juu yake.

19. Wewe, BWANA, unadumu milele;Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi.

20. Mbona watusahau sikuzote;Na kutuacha muda huu mwingi?

21. Ee BWANA, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale.

22. Isipokuwa wewe umetukataa kabisa;Nawe una hasira nyingi sana juu yetu.