48. Nikainama, nikamsujudia BWANA, nikamtukuza BWANA, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, aliyeniongoza njiani, nimtwalie mwana wa bwana wangu binti wa ndugu yake.
49. Basi, kama mnataka kumfanyia rehema na kweli bwana wangu, niambieni kama sivyo, niambieni; ili nigeuke upande wa kuume au wa kushoto.
50. Ndipo Labani na Bethueli wakajibu wakasema, Neno hili limetoka kwa BWANA, wala sisi hatuwezi kukuambia neno jema wala baya.
51. Tazama, huyo Rebeka yuko mbele yako, umchukue, ukaende zako awe mke wa mwana wa bwana wako, kama alivyosema BWANA.
52. Ikawa mtumishi wa Ibrahimu aliposikia maneno yao, akainama hata nchi mbele za BWANA.
53. Kisha huyo mtumishi akatoa vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi, akampa Rebeka; na vitu vya thamani akampa nduguye na mamaye pia.
54. Wakala wakanywa, yeye na watu waliokuwa pamoja naye, nao wakakaa usiku. Wakaondoka asubuhi, naye akasema, Nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu.
55. Ndugu yake na mama yake wakasema, Msichana na akae kwetu kama siku kumi, zisipungue, baadaye aende.
56. Naye akawaambia, Msinikawilishe, mradi BWANA amefanikisha njia yangu; nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu.
57. Wakasema, Na tumwite huyo msichana, tumwulize mwenyewe.
58. Wakamwita Rebeka wakamwuliza, Je! Utakwenda na mtu huyu? Akasema, Nitakwenda.
59. Ndipo wakampeleka Rebeka ndugu yao, na yaya wake, na mtumishi wa Ibrahimu, na watu wake.
60. Wakambarikia Rebeka, wakamwambia, Ndugu yetu, uwe wewe mama wa kumi elfu, mara elfu nyingi, na wazao wako waurithi mlango wa hao wawachukiao.