11. Busara ya mtu huiahirisha hasira yake;Nayo ni fahari yake kusamehe makosa.
12. Ghadhabu ya mfalme ni kama ngurumo ya simba;Bali hisani yake kama umande juu ya majani.
13. Mwana mpumbavu ni msiba kwa babaye;Na ugomvi wa mke kama kutona-tona daima.
14. Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye;Bali mke mwenye busara, mtu hupewa na BWANA.
15. Uvivu humtia mtu katika usingizi mzito;Na nafsi yake mvivu itaona njaa.
16. Yeye aihifadhiye amri huihifadhi nafsi yake;Bali yeye asiyeziangalia njia zake atakufa.
17. Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA;Naye atamlipa kwa tendo lake jema.
18. Mrudi mwanao, kwa maana liko tumaini;Wala usiikaze nafsi yako kwa kuangamia kwake.
19. Mtu wa hasira nyingi atachukua adhabu yake,Maana ujapomwokoa huna budi kufanya tena.
20. Sikiliza mashauri, ukapokee mafundisho,Upate kuwa na hekima siku zako za mwisho.
21. Mna hila nyingi moyoni mwa mtu;Lakini shauri la BWANA ndilo litakalosimama.
22. Haja ya mwanadamu ni hisani yake;Ni afadhali maskini kuliko mwongo.
23. Kumcha BWANA huelekea uhai;Atakaa ameshiba; hatajiliwa na ubaya.
24. Mtu mvivu hutia mkono wake sahanini;Ila hataki hata kuupeleka kinywani pake.
25. Mpige mwenye mzaha, na mjinga atapata busara;Mwonye mwenye ufahamu, naye atatambua maarifa.
26. Apotezaye mali za babaye na kumfukuza mamaye,Ni mwana aaibishaye, na kuleta lawama.
27. Mwanangu, acha kusikia mafundisho,Ukitaka tu kuyaasi maneno ya maarifa.