4. na ng’ombe mume, na kondoo mume, kwa sadaka za amani, ili kuwachinja mbele za BWANA; na sadaka ya unga uliochanganywa na mafuta; kwa maana, BWANA hivi leo atawatokea.
5. Nao wakayaleta hayo yaliyoagizwa na Musa wakayaweka mbele ya hema ya kukutania; kisha mkutano wote ukakaribia wakasimama mbele za BWANA.
6. Kisha Musa akasema, Neno aliloliagiza BWANA kwamba mlifanye ni hili; na huo utukufu wa BWANA utawatokea.
7. Musa akamwambia Haruni, Ikaribie madhabahu, uitoe sadaka yako ya dhambi, na sadaka yako ya kuteketezwa, ukafanye upatanisho kwa ajili ya nafsi yako, na kwa ajili ya watu; nawe uitoe hiyo dhabihu ya watu, ukafanye upatanisho kwa ajili yao; kama BWANA alivyoagiza.
8. Basi Haruni akakaribia madhabahuni, akamchinja huyo mwana-ng’ombe wa sadaka ya dhambi, aliyekuwa kwa ajili ya nafsi yake.
9. Kisha wana wa Haruni wakamsongezea Haruni ile damu; naye akatia kidole chake katika damu, na kuitia katika pembe za madhabahu, kisha akaimwaga hiyo damu hapo chini ya madhabahu;
10. lakini mafuta, na figo, na kitambi kilichotoka katika ini ya hiyo sadaka ya dhambi, akaviteketeza juu ya madhabahu, kama BWANA alivyomwagiza Musa.
11. Na nyama, na ngozi akazichoma moto nje ya marago.
12. Naye akaichinja sadaka ya kuteketezwa; na wanawe Haruni wakamsongezea ile damu, naye akainyunyiza katika madhabahu pande zote.
13. Nao wakamletea sadaka ya kuteketezwa kipande kwa kipande, na kichwa; naye akaviteketeza juu ya madhabahu.
14. Kisha akaosha matumbo, na miguu na kuiteketeza juu ya hiyo sadaka ya kuteketezwa madhabahuni.
15. Kisha akaisongeza dhabihu ya watu, akamtwaa mbuzi wa sadaka ya dhambi aliyekuwa kwa hao watu, na kumchinja, na kumtoa kwa ajili ya dhambi kama yule wa kwanza.