Law. 27:19-34 Swahili Union Version (SUV)

19. Na kama yeye aliyeliweka shamba wakfu akitaka kulikomboa kweli, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano ya hiyo fedha ya hesabu yako, nalo litathibitishwa kwake.

20. Lakini asipotaka kulikomboa shamba, au kama amemwuzia mtu mwingine hilo shamba, halitakombolewa tena kabisa;

21. ila hilo shamba litakuwa takatifu kwa BWANA litakapotoka katika yubile, kama ni shamba lililowekwa wakfu; litakuwa mali ya kuhani.

22. Tena kama akiweka wakfu kwa BWANA shamba ambalo amelinunua, ambalo si shamba la milki yake;

23. ndipo kuhani atamhesabia kima cha kuhesabu kwako hata mwaka wa yubile: naye atatoa siku hiyo kama hesabu yako, kuwa ni kitu kitakatifu kwa BWANA.

24. Mwaka wa yubile shamba hilo litarejea kwake huyo ambaye lilinunuliwa kwake, yaani, huyo ambaye nchi hiyo ni milki yake.

25. Na hesabu zako zote zitaandamana shekeli ya mahali patakatifu; gera ishirini zitakuwa shekeli moja.

26. Mzaliwa wa kwanza tu katika wanyama, aliyewekwa kuwa mzaliwa wa kwanza kwa BWANA, mtu awaye yote hatamweka kuwa mtakatifu; kama ni ng’ombe, kama ni kondoo, huyo ni wa BWANA.

27. Na kama ni wa mnyama asiye safi, ndipo atamkomboa kama hesabu yako ilivyo, naye ataongeza sehemu ya tano ya bei yake; au asipokombolewa, ndipo atauzwa kama hesabu yako ilivyo.

28. Pamoja na hayo, hakitauzwa wala kukombolewa kitu cho chote kilichowekwa wakfu, ambacho mtu amekiweka wakfu kwa BWANA, katika vitu vyote alivyo navyo, kama ni mtu, au mnyama, au kama ni shamba la milki yake; kila kitu kilichowekwa wakfu ni kitakatifu sana kwa BWANA.

29. Kila aliyewekwa wakfu, aliyewekwa wakfu na binadamu, hatakombolewa; sharti atauawa.

30. Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya BWANA; ni takatifu kwa BWANA.

31. Na kama mtu akitaka kukomboa cho chote cha zaka yake, ataongeza sehemu yake ya tano juu yake.

32. Tena zaka yote ya ng’ombe, au ya kondoo, kila apitaye chini ya fimbo; sehemu ya kumi watakuwa ni watakatifu kwa BWANA.

33. Hataangalia kwamba ni mwema au kwamba ni mbaya, wala hatambadili; na kama akimbadili na yo yote, ndipo wote wawili, huyo na huyo waliobadiliwa watakuwa ni watakatifu; hatakombolewa.

34. Haya ndiyo maagizo, BWANA aliyomwagiza Musa kwa ajili ya wana wa Israeli katika mlima wa Sinai.

Law. 27