4. Pamoja na hayo, wanyama hawa hamtawala katika wale wenye kucheua, na katika wale walio na kwato; ngamia, kwa sababu yuacheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu.
5. Na wibari, kwa sababu yeye hucheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu.
6. Na sungura, kwa sababu hucheua, lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu.
7. Na nguruwe, kwa sababu yeye anazo kwato, ni mwenye miguu iliyopasuka kati, lakini hacheui, yeye ni najisi kwenu.
8. Msiile nyama yao, wala msiiguse mizoga yao; hao ni najisi kwenu.
9. Katika hao wote walio ndani ya maji mtakula hawa; kila aliye na mapezi na magamba, ndani ya hayo maji, na ndani ya bahari, na ndani ya mito, mtakula hao.
10. Na hao wote wasio na mapezi na magamba, ndani ya bahari, na ndani ya mito, katika hao waendao majini, na katika wote wenye uhai, waliomo majini, hao ni machukizo kwenu,
11. watakuwa machukizo kwenu; msiile nyama yao, na mizoga yao itakuwa machukizo kwenu.
12. Kila asiye na mapezi wala magamba aliye ndani ya maji ni machukizo kwenu.
13. Kisha katika ndege hawa watakuwa ni machukizo kwenu; hawataliwa, ndio machukizo; tai, na furukombe, na kipungu;
14. na mwewe, na kozi kwa aina zake,
15. na kila kunguru kwa aina zake;
16. na mbuni, na kirukanjia, na dudumizi, na kipanga kwa aina zake;
17. na bundi, na mnandi, na bundi mkubwa;
18. na mumbi, na mwari, na mderi;
19. na korongo, na koikoi kwa aina zake, na hudihudi, na popo.
20. Tena vyote vitambaavyo vyenye mabawa viendavyo kwa miguu minne, hivi ni machukizo kwenu.
21. Pamoja na hayo, hivi vitambaavyo vyenye mabawa viendavyo kwa miguu minne ni halali kula, hao walio na miguu mirefu, ya kurukia juu ya nchi;
22. katika hao mna ruhusa kuwala; nzige kwa aina zake, na nzige kuu kwa aina zake, na panzi kwa aina zake, na parare kwa aina zake.
23. Lakini vyote vitambaavyo vyenye mabawa, vilivyo na miguu minne, ni machukizo kwenu.