15. Kama huyo mwenyewe alikuwapo pamoja na mnyama wake, hatalipa; kama ni mnyama aliyeajiriwa, alikwenda kwa ajili ya ujira wake.
16. Mtu akimshawishi mwanamwali, aliyeposwa na mume, na kulala naye, lazima atatoa mahari kwa ajili yake ili awe mkewe.
17. Ikiwa baba yake huyo mwanamwali akataa kabisa kumpa, atalipa fedha kama hesabu ya mahari ya mwanamwali ilivyo.
18. Usimwache mwanamke mchawi kuishi.
19. Mtu awaye yote alalaye na mnyama sharti atauawa.
20. Mtu atakayemchinjia sadaka mungu ye yote, isipokuwa ni yeye BWANA peke yake, na angamizwe kabisa.
21. Usimwonee mgeni, wala kumtendea jeuri; kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri.
22. Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima.
23. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao,
24. na hasira yangu itawaka moto, nami nitawaua ninyi kwa upanga; na wake wenu watakuwa wajane, na watoto wenu mayatima.
25. Ukimkopesha mtu aliye maskini, katika watu wangu walio pamoja nawe; usiwe kwake mfano wa mwenye kumdai; wala hutamwandikia faida.
26. Ikiwa wewe kwa njia yo yote wapokea nguo ya jirani yako rehani, lazima utamrudishia mbele ya jua kuchwa;
27. maana hiyo nguo ni kifuniko chake, hiyo peke yake ni nguo ya ngozi yake; je! Atalalia nini? Itakuwa, hapo atakaponililia mimi, nitasikia; kwa kuwa mimi ni mwenye rehema.
28. Usimtukane Mungu, wala usimlaani mkuu wa watu wako.
29. Usikawie kuleta malimbuko ya matunda yako na ya vinywaji vyako. Mzaliwa wa kwanza katika wanao waume utanipa mimi.
30. Nawe utafanya vivyo katika ng’ombe zako, na kondoo zako; utamwacha siku saba pamoja na mama yake; siku ya nane utanipa mimi.
31. Nanyi mtakuwa watu watakatifu kwangu mimi; kwa hiyo msiile nyama yo yote iliyoraruliwa huko kondeni na mnyama wa mwitu; mtawatupia mbwa nyama hiyo.