7. Mtu akimwuza binti yake awe kijakazi, hatatoka yeye kama watumwa wa kiume watokavyo.
8. Kwamba bwana wake hakupendezewa naye, akiwa amemposa, ndipo atakubali akombolewe; hana amri yeye kumwuza aende kwa watu wageni maana amemtenda kwa udanganyifu.
9. Kwamba amposa mwanawe, atamtendea kama desturi zipasazo binti zake.
10. Kwamba ajitwalia mke mwingine, chakula chake huyo, na nguo zake, na ngono yake, hatampunguzia.
11. Kwamba hamfanyii mambo haya matatu, ndipo atatoka aende bure, pasipo kutolewa mali.
12. Mtu awaye yote ampigaye mtu, hata akafa, hana budi atauawa huyo.
13. Lakini kama hakumvizia, ila Mungu amemtia mkononi mwake; basi nitakuonyesha mahali atakapopakimbilia.
14. Lakini, mtu akimwendea mwenziwe kwa kujikinai, kusudi apate kumwua kwa hila; huyo utamwondoa hata madhabahuni pangu, auawe.
15. Ampigaye baba yake au mama yake, sharti atauawa.
16. Yeye amwibaye mtu, na kumwuza, au akipatikana mkononi mwake, sharti atauawa huyo
17. Yeye amwapizaye baba yake au mama yake, sharti atauawa.
18. Watu wakigombana, na mmoja akimpiga mwenziwe kwa jiwe, au kwa konde, asife, lakini yualazwa kitandani mwake;
19. atakapoinuka tena na kuenenda nje kwa kutegemea fimbo, ndipo hapo yule aliyempiga ataachwa; ila atamlipa kwa ajili ya hayo majira yake yaliyompotea, naye atamwuguza hata apone kabisa.
20. Mtu akimpiga mtumwa wake, au kijakazi chake, kwa fimbo, naye akifa mkononi mwake, hana budi ataadhibiwa.
21. Lakini akipona siku moja au mbili hataadhibiwa; maana, ni mali yake.
22. Watu waume wakiteta pamoja, wakamwumiza mwanamke mwenye mimba hata akaharibu mimba, tena yasiwe madhara zaidi; sharti atatozwa mali kama atakavyomwandikia mumewe huyo mwanamke; atalipa kama hao waamuzi watakavyosema.
23. Lakini kwamba pana madhara zaidi, ndipo utatoza uhai kwa uhai,
24. jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu,
25. kuteketeza kwa kuteketeza, jeraha kwa jeraha, chubuko kwa ajili ya chubuko.
26. Mtu akimpiga mtumwa wake jicho, au jicho la kijakazi chake, na kuliharibu; atamwacha huru kwa ajili ya jicho lake.