Kum. 18:3-13 Swahili Union Version (SUV)

3. Na hii itakuwa haki ya makuhani kwa watu hao wasongezao sadaka, ikiwa ni ng’ombe au kondoo wampe kuhani mkono, na mashavu mawili, na tumbo.

4. Malimbuko ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na manyoya ya kwanza ya kondoo zako, umpe.

5. Kwani BWANA, Mungu wako, amemchagua katika kabila zako zote, asimame atumike kwa jina la BWANA, yeye na wanawe milele.

6. Na akija Mlawi atokaye katika malango yako mojawapo, katika Israeli yote alipokuwa akikaa, akaja kwa mapenzi yote ya nafsi yake mahali atakapochagua BWANA;

7. na atumike kwa jina la BWANA, Mungu wake, kama wafanyavyo ndugu zake wote, Walawi wasimamao huko mbele za BWANA.

8. Wawe na fungu sawasawa la kula, pamoja na haya yaliyomfikilia kwa kuuzwa urithi wa baba zake.

9. Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo BWANA, Mungu wako usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale.

10. Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri,

11. wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.

12. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA; kisha ni kwa sababu ya hayo BWANA, Mungu wako, anawafukuza mbele yako.

13. Uwe mkamilifu kwa BWANA, Mungu wako.

Kum. 18