Kum. 18:1-9 Swahili Union Version (SUV)

1. Makuhani Walawi, kabila yote ya Lawi, wasiwe na fungu wala urithi pamoja na Israeli; watakula sadaka za BWANA zifanywazo kwa moto, na urithi wake.

2. Wala wasiwe na urithi kati ya ndugu zao; BWANA ndiye urithi wao, kama alivyowaambia.

3. Na hii itakuwa haki ya makuhani kwa watu hao wasongezao sadaka, ikiwa ni ng’ombe au kondoo wampe kuhani mkono, na mashavu mawili, na tumbo.

4. Malimbuko ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na manyoya ya kwanza ya kondoo zako, umpe.

5. Kwani BWANA, Mungu wako, amemchagua katika kabila zako zote, asimame atumike kwa jina la BWANA, yeye na wanawe milele.

6. Na akija Mlawi atokaye katika malango yako mojawapo, katika Israeli yote alipokuwa akikaa, akaja kwa mapenzi yote ya nafsi yake mahali atakapochagua BWANA;

7. na atumike kwa jina la BWANA, Mungu wake, kama wafanyavyo ndugu zake wote, Walawi wasimamao huko mbele za BWANA.

8. Wawe na fungu sawasawa la kula, pamoja na haya yaliyomfikilia kwa kuuzwa urithi wa baba zake.

9. Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo BWANA, Mungu wako usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale.

Kum. 18