Hes. 15:12-26 Swahili Union Version (SUV)

12. Kama hesabu ilivyo ya hao mtakaowaandaa, ndivyo mtakavyofanya kwa kila mmoja, sawasawa na hesabu yao.

13. Wote ambao wamezaliwa kwenu watafanya hayo yote kwa kuandama mfano huo, katika kusongeza sadaka kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa BWANA.

14. Tena kwamba mgeni amekaa kwenu, au mtu ye yote aliye kati yenu katika vizazi vyenu, naye yuataka kusongeza sadaka kwa moto, na harufu ya kupendeza kwa BWANA; kama ninyi mfanyavyo, na yeye atafanya vivyo.

15. Katika huo mkutano, kutakuwa na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye pamoja nanyi; ni amri ya milele katika vizazi vyenu; kama ninyi mlivyo, na mgeni atakuwa vivyo mbele za BWANA.

16. Itakuwa sheria moja na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye nanyi.

17. Kisha BWANA akanena na Musa, na kumwambia,

18. Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapoingia nchi niwapelekayo,

19. ndipo itakapokuwa ya kwamba hapo mtakapokula katika chakula cha nchi hiyo, mtamsongezea BWANA sadaka ya kuinuliwa.

20. Katika unga wenu wa kwanza wa chenga-chenga mtasongeza mkate uwe sadaka ya kuinuliwa; vile vile kama mfanyavyo sadaka ya kuinuliwa ya sakafu ya kupuria nafaka, ndivyo mtakavyoiinua.

21. Malimbuko ya unga wenu mtampa BWANA sadaka ya kuinuliwa, katika vizazi vyenu.

22. Tena mtakapokosa, msiyashike maagizo hayo yote BWANA aliyomwambia Musa,

23. hayo yote BWANA aliyowaagiza kwa mkono wa Musa, tangu siku hiyo BWANA aliyoleta maagizo, na baadaye katika vizazi vyenu

24. ndipo itakapokuwa, kama ni kosa lililofanywa pasipo kujua, wala mkutano haukuwa na fahamu, ndipo mkutano wote utasongeza ng’ombe mume mmoja mdogo kuwa sadaka ya kuteketezwa, kuwa harufu ya kupendeza kwa BWANA, pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji, kama amri ilivyo, na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi.

25. Naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya mkutano wote wa wana wa Israeli, nao watasamehewa; maana, lilikuwa ni kosa, nao wamekwisha leta matoleo yao, sadaka iliyosongezwa kwa BWANA kwa moto, na sadaka yao ya dhambi pia wameileta mbele za BWANA kwa ajili ya kosa lao;

26. nao mkutano wote wa wana wa Israeli watasamehewa, na mgeni akaaye kati yao; maana, katika habari za hao wote jambo hilo lilitendeka pasipo kujua.

Hes. 15