21. Kisha yule mtu, Elkana, na watu wote wa nyumbani mwake, wakakwea kwenda kumtolea BWANA dhabihu ya mwaka, na nadhiri yake.
22. Bali Hana hakukwea; maana alimwambia mumewe, Sitakwea mimi hata mtoto wangu atakapoachishwa maziwa, hapo ndipo nitakapomleta, ili ahudhurie mbele za BWANA, akae huko daima.
23. Elkana, mumewe, akamwambia, Haya, fanya uonavyo vema; ngoja hata utakapomwachisha maziwa; BWANA na alithibitishe neno lake tu. Basi yule mwanamke akangoja, akamnyonyesha mtoto wake, hata akamwachisha maziwa.
24. Naye alipokuwa amekwisha kumwachisha maziwa, akamchukua pamoja naye, na ng’ombe watatu, na efa moja ya unga, na chupa ya divai, akamleta nyumbani kwa BWANA, huko Shilo; na yule mtoto alikuwa mtoto mdogo.
25. Nao wakamchinja huyo ng’ombe, wakamleta mtoto kwa Eli.
26. Akasema, Ee bwana wangu, kama iishivyo roho yako, bwana wangu, mimi ndimi yule mwanamke aliyesimama karibu nawe hapa, nikimwomba BWANA.
27. Naliomba nipewe mtoto huyu; BWANA akanipa dua yangu niliyomwomba;
28. kwa sababu hiyo mimi nami nimempa BWANA mtoto huyu; wakati wote atakaokuwa hai amepewa BWANA. Naye akamwabudu BWANA huko.