5. Basi, wakaanza kumnungunikia Mungu na Mose, wakisema, “Kwa nini mmetutoa Misri tuje tukafie humu jangwani? Humu hamna chakula wala maji; nasi tumechoshwa na chakula hiki duni.”
6. Hapo Mwenyezi-Mungu akapeleka nyoka wenye sumu miongoni mwa watu, wakawauma hata Waisraeli wengi wakafa.
7. Basi, watu wakamwendea Mose, wakamwambia, “Tumetenda dhambi kwa kumnungunikia Mwenyezi-Mungu na wewe pia. Mwombe Mwenyezi-Mungu atuondolee nyoka hawa.” Kwa hiyo, Mose akawaombea watu.
8. Ndipo Naye Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Tengeneza nyoka wa shaba, umtundike juu ya mlingoti. Mtu yeyote atakayeumwa na nyoka, akimtazama nyoka huyo wa shaba, atapona.”
9. Basi, Mose akatengeneza nyoka wa shaba, akamtundika juu ya mlingoti. Kila mtu aliyeumwa na nyoka alipomtazama nyoka huyo wa shaba, alipona.
10. Waisraeli waliendelea na safari yao, wakapiga kambi huko Obothi.
11. Kutoka huko walisafiri mpaka Iye-abarimu, katika jangwa upande wa mashariki, mwa Moabu.
12. Kutoka huko walisafiri wakapiga kambi yao katika bonde la Zeredi.
13. Kutoka huko walisafiri, wakapiga kambi kaskazini ya mto Arnoni, ambao hutiririka kutoka katika nchi ya Waamori na kupitia jangwani. Mto Arnoni ulikuwa mpaka kati ya Wamoabu na Waamori.
14. Kwa sababu hiyo, imeandikwa katika kitabu cha vita vya Mwenyezi-Mungu:“Mji wa Wahebu nchini Sufa,na mabonde ya Arnoni,
15. na mteremko wa mabondeunaofika hadi mji wa Ari,na kuelekea mpakani mwa Moabu!”
16. Kutoka huko Waisraeli walisafiri mpaka Beeri; yaani kisima ambapo Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Wakusanyeni watu pamoja, nami nitawapa maji.”
17. Hapo Waisraeli waliimba wimbo huu:“Bubujika maji ee kisima! – Kiimbieni!
18. Kisima kilichochimbwa na wakuukilichochimbwa sana na wenye cheo,kwa fimbo zao za enzi na bakora.”Kutoka jangwani walisafiri mpaka Matana,
19. kutoka Matana mpaka Nahalieli, kutoka Nahalieli mpaka Bamothi,
20. na kutoka Bamothi mpaka kwenye bonde linaloingia nchi ya Moabu, kwenye kilele cha Mlima Pisga, kielekeacho chini jangwani.
21. Waisraeli walimpelekea mfalme Sihoni wa Waamori, ujumbe huu:
22. “Turuhusu tupite katika nchi yako; hatutakwenda pembeni na kuingia mashambani au katika mashamba ya mizabibu, wala hatutakunywa maji ya visima vyenu; tutapita moja kwa moja katika barabara kuu ya mfalme mpaka tumeondoka nchini mwako.”