Hesabu 15:29-40 Biblia Habari Njema (BHN)

29. Mtafuata sheria moja kila mtu atakayekosea bila kukusudia, awe ni mwananchi Mwisraeli au ni mgeni anayeishi pamoja nanyi.

30. “Lakini mtu yeyote atakayekosa kwa makusudi, awe mwananchi au mgeni, atakuwa anamdhihaki Mwenyezi-Mungu, na ni lazima akatiliwe mbali miongoni mwa watu wake.

31. Maana amekataa yale aliyosema Mwenyezi-Mungu na kuvunja mojawapo ya amri zake. Mtu huyo atakatiliwa mbali kabisa; na lawama ya kifo chake itakuwa juu yake mwenyewe.”

32. Siku moja, wakati Waisraeli walipokuwa jangwani, walimwona mtu mmoja akiokota kuni siku ya Sabato.

33. Basi, mtu huyo akapelekwa mbele ya Mose, Aroni na jumuiya yote.

34. Wao wakamweka kifungoni kwa sababu haikuwa bado imesemwa wazi namna ya kumfanya mtu wa namna hiyo.

35. Ndipo Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Mtu huyo lazima auawe; jumuiya yote itampiga mawe nje ya kambi.”

36. Basi, watu wakamtoa nje ya kambi, wakampiga mawe mpaka akafa, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

37. Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose:

38. “Waambie watu wa Israeli, uwaagize wajifanyie vishada katika ncha za mavazi yao, na kutia nyuzi za buluu juu ya kila kishada. Waambie wafanye hivyo katika vizazi vyao vyote vijavyo.

39. Vishada hivyo vitakuwa kumbukumbu kwenu. Kila mtakapoviona, mtazikumbuka amri zangu zote na kuzifuata, ili msije mkafuata matakwa yenu na yale mnayoyaona kwa macho yenu wenyewe.

40. Vishada hivyo vitawakumbusha amri zangu zote na mtazifuata zote kikamilifu, nanyi mtakuwa watakatifu wangu.

Hesabu 15